Numbers 17

Kuchipuka Kwa Fimbo Ya Haruni

1 Bwana akamwambia Musa, 2 a“Sema na Waisraeli, na ujipatie fimbo kumi na mbili kutoka kwao, moja kutoka kwa kila mmoja wa viongozi wa kabila za baba zao. Andika jina la kila mtu kwenye fimbo yake. 3 bKwenye fimbo ya Lawi andika jina la Haruni, kwa maana ni lazima iwepo fimbo moja kwa kila kiongozi kwa ajili ya kila kabila la baba zao. 4 cZiweke hizo fimbo ndani ya Hema la Kukutania mbele ya Sanduku la Ushuhuda, mahali nikutanapo nawe. 5 dFimbo ya mtu nitakayemchagua itachipuka, nami mwenyewe nitayakomesha haya manung’uniko ya mara kwa mara ya Waisraeli dhidi yako.”

6Hivyo Musa akasema na Waisraeli, nao viongozi wao wakampa fimbo kumi na mbili, fimbo moja kwa ajili ya kila kabila la baba zao, nayo fimbo ya Haruni ikiwa miongoni mwa hizo. 7 eMusa akaziweka hizo fimbo mbele za Bwana ndani ya Hema la Ushuhuda.

8 fSiku iliyofuata Musa aliingia kwenye Hema la Ushuhuda akaona ile fimbo ya Haruni ambayo iliwakilisha jamaa ya Lawi haikuwa tu imechipuka, bali pia ilikuwa imetoa machipukizi, kuchanua maua na kuzaa malozi. 9Ndipo Musa akaleta zile fimbo zote kwa Waisraeli wote kutoka mbele za Bwana. Wakaziangalia, na kila mtu akaichukua fimbo yake mwenyewe.

10 g Bwana akamwambia Musa, “Rudisha fimbo ya Haruni mbele ya Sanduku la Ushuhuda, ili ihifadhiwe kama alama kwa waasi. Hili litakomesha manung’uniko yao dhidi yangu, ili kwamba wasife.” 11Musa akafanya kama Bwana alivyomwamuru.

12 hWaisraeli wakamwambia Musa, “Tutakufa! Tumepotea, sote tumepotea! 13 iYeyote akaribiaye Maskani ya Bwana atakufa. Je, sisi sote tutakufa?”
Copyright information for SwhKC